Jumatatu, 4 Aprili 2016

Unapojaribiwa Jiandae Kupambana Na Majaribu Hayo!!!

 
Nakuchukua nafasi hii kukukaribisha kwenye ulingo huu wa kujifunza maana kujifunza hakuzeeki, unatakiwa kujifunza siku zote katika maisha yako. Kila kitu unachokiona kinakufundisha jambo fulani, kama hujui kinakufundisha nini ni kwa sababu macho yako hayajafumbuliwa upate kufahamu unachojifunza kutoka kwenye vitu hivyo.
 
Leo nakuletea makala hii kwa lengo la kukufumbua macho yako na akili yako ili uweze kugundua kitu gani kinakukwamisha ili uchukue hatua haraka kulitatua tatizo hilo na hatimaye uendelee vema na safari yako ya kuelekea mafanikio makubwa.

Majaribu ni nini?
Neno majaribu mara nyingi hutumiwa sana kwenye upande wa dini, kuelezea hali ngumu inayompata mtu agharabu kwa lengo la kumjaribu uimara wa imani yake. Kwa kifupi majaribu ni hali au kitu ambacho huwa mzigo mzito unaomwandama mwanadamu. Huko kwenye dini tunaambiwa mtu anapojaribiwa na akalishinda jaribu linalomsumbua hupewa thawabu na Mwenyezi Mungu kama tuzo ya kufuzu mafunzo anayotaka Mungu amfundishe mtu huyo.

Katika makala hii, nataka tulizumgumzie neno majaribu kuelezea magumu yote unayokumbana nayo wakati unapotaka kuelekea mafanikio yako makubwa. 
 
Kwa mfano, unataka uanzishe biashara yako lakini huna mtaji, umefanya kila njia kutafuta mtaji lakini umekosa hilo ni jaribu moja wapo. Mfano mwingine unasoma shuleni au chuoni lakini  kadri siku zinavyokwenda hufanyi vizuri darasani umejaribu kila mbinu lakini bado huoni matumaini,  hilo limeshageuka kuwa jaribu lako. 
 
Unaweza kuwa unafamilia yako lakini kutokana na hali ngumu ya maisha, huna pesa na familia hiyo inahitaji pesa kwa kiwango kikubwa lakini bado huoni mahali pa kutokea, hilo nalo limeshakuwa jaribu lako. Sio hayo tu na mengine mengi magumu unayoyapitia labda kwenye swala la mahusiano na mwenzi wako, uhusiano wenu umelegalega kwa siku nyingi uaminifu kati yenu umepungua na kuna kila dalili za kusalitiana, nalo hilo limekuwa jaribu kwako.
 
Kama unamazingira kama hayo au yanakaribiana na hayo basi somo hili ni lakwako. Tuendelee kujifunza na baada ya somo hili unaweza kupata nguvu mpya ya kushinda majaribu yako.

Usipogundua kama Tatizo Ulilonalo Ni Jaribu Huwezi Kushinda.
Wataalamu wa afya, kwa maana ya madaktari na wahudumu wengine wa afya hawawezi kumpa dawa mgonjwa bila kujiridhisha ugonjwa anaoumwa mgonjwa yule. 
 
Mambo hayo hayaishii huko tu hospitalini lakini hata katika maisha yetu ya kawaida bila kufahamu tatizo linalokusumbua sio rahisi kulishinda tatizo hilo. Kwa kuongezea zaidi bila kugundua kama changamoto uliyonayo ni jaribu huwezi kuishinda changamoto hiyo.

Dalili Hizi Zinakusaidia Kutambua kama Changamoto Uliyonayo Ni Jaribu
Kwa kawaida sio rahisi kugundua changamoto uliyonayo kama ni jaribu. Lakini ukitulia na kutafakari unaweza kufahamu kwamba changamoto inayokubili  ni jaribu. Dalili tatu zifuatazo zinaweza kutumika kukukufahamisha kwamba changamoto uliyonayo  ni jaribu.

Dalili ya kwanza: Kubwa mno huoni mahali pa kutokea, hakuna mtu wa kukusaidia unakata tamaa na kunyong’onyea. Hii ni moja ya dalili kwamba changamoto inayokukabili ni jaribu.

Dalili ya pili: Umesumbuka kwa muda mrefu huitaki hali ile au swala hilo lakini kila unapotaka kuishinda hali hiyo huwezi. Hii nayo ni moja ya dalili kwamba changamoto inayokusumbua ni jaribu. Mfano inaweza kuwa ni tabia Fulani mbaya kila unapojaribu kuiacha unajikuta umerudia tena na tena mpaka inafikia hatua umekosa raha na hujui utatokaje.

Dalili ya tatu: Chanzo chake sio wewe ni watu wengine, ndugu na jamaa zako wa karibu  ndio wanaokutesa kwa aina moja au nyingine tena kwa muda mrefu. Ukiona hivyo ujue hilo linaweza kuwa jaribu lako.

Umegundua Jaribu Lako? Jiandae
Kama nilivyoanza kukueleza hapo juu, mgonjwa akienda hospitali jambo la kwanza ni kujua ugonjwa anaoumwa ndipo apewe dawa sahihi ya kutibu ugonjwa huo. Tukirudi kwenye somo letu, unapogundua kwamba changamoto inayokukabili ni jaribu unatakiwa ujiandae. Ujiandae kufanya nini?, ujiandae kushinda jaribu hilo.
 
Binadamu tumeumbwa kwa namna ya ajabu sana, unapogundua tatizo linalokusumbua mara nyingi huwa tunapata nguvu na ujasiri wa kukabiliana na tatizo hilo, tunapataje nguvu?, “ Tunapata nguvu kutoka kwenye kitu kinachoitwa kujitambua “awareness” . 
 
Don Miguel Ruiz anasema katika kitabu chake The Mastery of Love , kujitambua “awareness” ni silaha ya kwanza kushinda kila aina ya uongo na hisia mbaya. 
 
Mfano ukiwa na “awareness” kama kuna mtu anakutukana ukitaka kumrudishia kwa matusi hutaweza maana utakumbuka nikimrudishia kwa matusi kuna kupigana au kujenga uhasama. Badala yake utakaa kimya. Lakini bila “awareness” lazima utamrudishia matusi na maneno mengine mengi. 
 
Umakini (awareness), ni silaha kubwa sana ya kukupa uvumilivu na hekima ya kuamua vema kwa sababu ukiwa na “awareness” hutataka umkwaze mtu.

Lazima Ushinde Jaribu Lako.
Weka nia ya dhati ya kushinda jaribu lako. Tumia “Umakini”ili usimkwaze mtu. Kumbuka unaposhinda jaribu lazima upate tuzo. Soma kitabu cha Ayubu jinsi alivyopambana na majaribu yake hadi akashinda na hatimaye akapewa tuzo kubwa. Soma kitabu cha Ayubu kwenye biblia sura ya 1,2 na sura ya 42.

Jaribu Linapokushinda Unapoteza Kila Kitu.
Hata kile kidogo ulichonacho kitapotea kama jaribu utaliruhusu likushinde. Usikubali kushindwa na jaribu, pambana ulishinde halafu baada ya ushindi lazima utapata tuzo kubwa. Ndio maana wajasiriamali wanaoshinda majaribu yao wanapewa tuzo ya kufanikiwa kimaisha. Tunawaona wakiishi maisha mazuri ya utajiri mwingi. Ni kwa sababu wanashinda majaribu yao. Nakuhimiza tena unapogundua jaribu lako, jiandae kushinda jaribu hilo.

Nakutakia Maandalizi Mema Ya Safari Yako Ya Kupambana Na Majaribu yako!!!

0 comments: