Jumatano, 30 Machi 2016

Je Unaijua Talanta (Karama) Yako?

  

Unaweza kuwa unawafahamu watu wengi sana ambao wanaweka juhudi kubwa katika kufanya kitu au jambo fulani, Wanatumia ujuzi, muda, maarifa na rasilimali nyinginezo, Lakini bado hawafanikiwi!
Na kuna wengine wanafanya kitu kile kile na kwa juhudi zizo hizo na wanafanikiwa, tena kwa haraka zaidi!
Leo nimeonelea tujaribu kutafakari juu ya Talanta (Talent) au Karama jinsi zinavyohusika katika kutuletea mafanikio. Na inawezekana unajiuliza ni vipi unaweza kuijua Talanta/Kalama yako?
Naomba tujiulize maswali haya machache kisha tutapata kufahamu jibu la swali lako.

1. Ikiwa kuna maua ya rangi mbalimbali, kuna mekundu, meupe, ya njano na     kadhalika, je, ua jekundu linajuaje kama lenyewe ni jekundu na ndiyo maana linatoa maua mekundu badala ya meupe?

 2. Kuna aina nyingi sana za mimea hapa duniani, mpunga na ngano kwa kiasi fulani zinafanana, sasa, kwanini mpunga huzaa mpunga badala ya ngano na ngano huzaa ngano badala ya mpunga?

3.Umekwisha wahi kujiuliza kwanini nyuki anauwezo wa kukuuma na kukusababishia maumivu makali?, unafikiri nani alimfundisha nyuki kuuma au aliipata wapi karama ya kuuma namna ile?
4.Unafikiri nani alimfundisha nyani kuruka ruka kwenye miti? Hiyo karama ya kuruka kwenye miti aliijuaje na kwa nini asiwe kama
swala ambaye hajui kuruka kwenye miti?

Hayo ni maswali machache yanayokufikirisha kidogo tunapoenda kutambua karama ya kila mtu iko wapi au ataijuaje. Ukitafakari kwa makini maswali hayo hapo juu utaona kwamba kumbe karama ya mtu na karama za wanyama na mimea imo ndani ya mnyama mwenyewe, imo ndani ya mmea wenyewe na imo ndani ya binadamu mwenyewe.
Chukulia kwa mfano maua; kila mti wa maua ndani yake kuna kitu ambacho kimefichwa hukioni kwa macho kinachouongoza mmea huo kutoa maua mekundu badala ya meupe. Vivyo hivyo kwa wanyama na viumbe wengine.

Kama Ni Hivyo Karama Ni Nini Basi?
Kwa lugha rahisi kabisa, naweza kusema karama ni mbegu ambayo mtu huwekewa tangu akiwa tumboni mwa mama yake ambayo humwezesha mtu huyo kufanya kazi au jambo fulani kwa njia ya kipekee na kwa urahisi tofauti na mtu mwingine. 

Mungu humwekea mbegu hii kila mtu na anapozaliwa akiamua kuifahamu mbegu ya karama aliyowekewa anaweza kuifahamu tena vizuri kabisa. Mbegu ya karama inaweza kustawi vizuri ikimwagiliwa na kutunzwa vizuri lakini pia inaweza kudumaa na hata kufa kabisa isipotunzwa vizuri. 

Kuitunza au kuimwagilia mbegu ya karama ni pale unapofanyia mazoezi au unapoitumia karama hiyo ndipo inapositawi na kuchanua vizuri zaidi.

Kila Mtu Anaweza Kuimba Lakini……
Ukichukulia kwa mfano, kundi la watu watano, na mmoja wao kati ya hao watano anakarama (kipaji) ya uimbaji, haijalishi mwalimu anayefundisha kuimba atafundisha kwa  aina gani lakini mwenye karama ya uimbaji ataimba vizuri zaidi kuliko wengine. 

Maana yake anayeimba siyo yeye bali ni karama inaimba ndani yake. Naweza kuongea kwa lugha ya ndani kidogo kwamba karama ni software ambayo mtu anakuwa nayo au anaweza kuitafuta halafu akaiingiza ndani yake na ikafanya kazi ile ile aliyokusudia mtu huyo imfanyie.

Kwa lugha ya kompyuta tunaweza kusema mwili wote wa binadamu ni windows kwahiyo unaweza ku-install program nyingine nyingi ndani ya windows hiyo. Kompyuta moja yenye windows kwa mfano windows 7 unaweza ku-install program nyingi sana na kila program inafanya kazi ile tu inayohusiana na progamu hiyo.

Mwili wa binadamu umetengenezwa kwa mfumo huo wenyewe kwa asili yake umewekewa mbegu ya karama lakini unaweza kujifunza karama nyingine hata mbili halafu zote zikawa karama zako japo hukuzaliwa nazo. Lakini karama zote unazoziweka wewe mwenyewe ndani yako kwa kujifunza haziwezi kuifikia ile karama ya asili kwa ubora. 

Unaweza kutumia nguvu nyingi sana kufanya kazi ambayo siyo karama yako lakini ukifanya kazi ambayo ni karama yako kazi huwa nyepesi zaidi.

Unawezaje Kuitambua Karama Yako?
Mtu anapozaliwa huwa na karama yake ya asili ambayo mimi naiita mbegu ya karama. Mtoto mdogo wa kuanzia miaka 5 hadi  miaka 18 huishi kwa karama yake ya asili. 

Umri wa kugundua karama ya mtu ni pale anapokuwa na miaka mitano hadi kumi na nane. Kwahiyo ukitaka kufahamu karama yako ni ipi jichunguze ulipokuwa na umri wa miaka mitano hadi kumi na nane ulikuwa unapenda kufanya mambo gani? Ulikuwa na ndoto za kuwa nani na michezo yako yote ilikuwa inahusu nini? Ukitafakari utapata jibu na  utapata kufahamu karama yako ni ipi. 

Ukifikia umri wa miaka kumi na nane na kuendelea ni vigumu kutambua karama yako,  pia ni vigumu kuiishi karama yako ikiwa huifahamu. Kuna mambo mengi hujitokeza ambayo huvuruga akili na wakati mwingine kuiua kabisa mbegu ya karama yako. Mambo hayo ni kama vile masomo, mapenzi, maisha magumu, kazi, mitindo ya ulimwengu na kadhalika. 

Mambo hayo humfanya mtu aipoteze karama yake ikiwa hakujipanga kuitumia vizuri tangu mwanzo.

Mambo Mawili Ya Kugundua Karama Yako

Jambo la kwanza: Chukua karatasi orodhesha mambo yote uliyokuwa unapenda kuyafanya katika umri wa miaka mitano hadi miaka kumi na nane. 

Hapo utaweza kuigundua mbegu ya karama yako jinsi ilivyokuwa inakusukuma uitumie lakini hukuelewa badala yake ukaanza kuiga karama za watu wengine ambazo sio za kwako na muda sio mrefu utashaangaa yale uliyokuwa unayaiga yanapotea halafu unabaki huna msimamo wa nini cha kufanya. 

Karama yako halisi inadalili moja kuu, hukupa furaha kila unapofanya kazi ya karama hiyo. Haijalishi ni kazi ngumu namna gani lakini utajikuta kila mara au kila siku unapenda kufanya jambo fulani tena kwa furaha kubwa, hiyo ni mbegu ya karama yako kama ulikuwa huitumii anza kuifufua haraka itakusaidia.

Jambo la pili: Nenda maktaba ya vitabu angalia ni vitabu gani unapenda kusoma?. Jichunguze kupitia vitabu utagundua kabisa moyo wako unataka nini usome, kila mara utakuwa ukiingia maktaba unajisikia hamu kusoma vitabu vya aina fulani na unapovisoma unafurahi kweli kweli, hiyo ni karama yako. Ukiigundua anza kuifufua mapema itakusaidia.

Karama Na Utajiri
Karama kwa jina jingine inaitwa Talanta au kipaji. Kwa nchi zilizoendelea watu wengi wameshafahamu namna ya kugundua karama ama vipaji vya watoto wao. Ndiyo maana wazazi wakishafahamu karama ya mtoto wao wanampeleka shule ya malezi ya karama hiyo. 

Kutokana na hilo mpaka sasa tunapata watu wengi mashuhuri kama akina Messi, Christian Ronaldo na wengine wengi kwa sababu karama zao zilimwagiliwa tangu mwanzo mpaka sasa zimestawi sana. 

Kwa mawazo yangu na maoni yangu, karama ama kipaji kinalipa sana ukikitumia vizuri. Haijalishi ni kipaji cha aina gani ilimradi kiwe kipaji kizuri tu ukikitumia vizuri unaweza kutajirika haraka sana. 

Hapa Tanzania bila shaka unayo mifano mingi ya watu waliotajirika kwa sababu ya kutumia vipaji vyao sawasawa. Mfano kwenye soka wapo, kwenye muziki wapo wengi na kila sehemu wapo wengi.

Taaluma Unayosomea Chuoni Inaweza Isiwe Karama Yako!
Kuna watu ama kwa kushawishiwa na ndugu zao ama kwa kuangalia pesa nyingi, wamejikuta wakisomea fani ambazo sio karama zao. Watu hao mioyoni mwao hawana amani hata kama wanapata pesa nyingi. 

Mimi nakushauri hata kama umesomea kazi ambayo sio karama yako (yaani huipendi) bado unayo nafasi ya kuitumia karama yako kuanzia sasa. Amua kuitumia karama yako ya asili utafurahia maisha.
Mwisho kwa leo, nakushauri uitafute karama yako mapema ili ukusaidie wakati huu kwenye maisha yako. Ukiigundua karama yako ichochee utafanya mambo makubwa sana.

0 comments: