“Nyimbo nzuri
zinazosikika ni tamu lakini nyimbo nzuri zisizosikika ni tamu zaidi”.
Hayo ni maneno yake John Keats, mtunzi mashuhuri wa
mashairi kutoka Uingereza. Mtunzi huyu anataka tufahamu kuwa maneno yale
yanayotoka kinywani mwa mtu na kusikika si yale yaliyomo ndani ya mtu huyo,
maana yale yanayotoka nje ya mtu hayawezi kumfanya mtu awe jinsi alivyo bali
maneno yale yanayosema kwa sauti ya chini isiyosikika ndiyo yanamfanya mtu awe
jinsi alivyo. Hali hii ni dhahiri kabisa katika maisha yetu.
Mara nyingi watu
wanapenda waonekane wazuri na wenye jambo jema wakiwa mbele za watu, husema kwa
namna ya kujisifia katika mambo fulani fulani ili mradi tu waonekane wema.
Lakini ukweli ni kwamba ndani ya watu hawa huwa kuna maneno yanayosikika kwa
sauti ya chini chini yakimsema mtu huyo
jinsi alivyo, haya maneno ndiyo yanayomfanya mtu awe jinsi alivyo kuanzia
tabia, sura yake, mwenendo wake wa kila siku na hali yake ya mahusiano na watu
wengine, wakati mwingine huathiri afya ya mtu huyo.
Mtu
Mmoja Ni Watu Wengi Ndani Yake.
Usishangae ndivyo ukweli ulivyo, ndani ya mtu mmoja
kuna mawazo zaidi ya maelfu kadhaa yanayopita kila wakati na kila wazo
linaongea maneno yake.
Don Miguel Luiz anayaita mawazo hayo watu wengi. Mawazo yale yanayopita mara
kwa mara ndani ya mtu ndiyo yanayotengeneza fikira ya mtu hiyo. Fikira ni
mkusanyiko wa mawazo ya muda mrefu ndani ya mtu yanayofanya tabia ya mtu huyo iwe
jinsi ilivyo.
Tabia za mtu zinajengwa na mawazo hayo na ikitokea kila wazo
linaongea bila kumsikiliza mwenzake huwa hakuna maelewano ndani ya mtu huyo na
hali hiyo huitwa msongo wa mawazo.
Tabia ya mtu na
kanuni zake za kuishi zinatengenezwa kwa namna hii ya mawazo kupita ndani yake.
Mawazo yale yanayopita mara kwa mara hutengeneza fikira na fikira ya mtu
hutengeneza tabia. Hivyo mtu huishi kwa kufuata fikira na tabia hizo. Sasa,
tabia hizo zinaweza kuwa nzuri au mbaya kwenye kila hali, mfano kwenye swala la
afya, akili,mahusiano, familia nk.
Utoaji
Wa Maamuzi Yako.
Umekuwa ukifanya maamuzi yako kwa namna gani punde
unapokutana na jambo linalohitaji kufanyiwa maamuzi? Mfano kwenye biashara
yako, masomo yako, kwenye mahusiano yako, kwenye kuchukua hatua za mafanikio
yako nk.
Namna unavyofanya maamuzi ndiyo tabia yako ilivyo kwenye swala la
maamuzi yako. Kama huwa unatoa maamuzi kwa jaziba haraka haraka je,
umeshagundua inakuletea madhara gani?
Mara nyingi mtu anayetoa maamuzi haraka
haraka baadae akija kutulia hugundua kuwa uamuzi wake haukuwa sahihi na mara
nyingi hujuta au hupata gharama kubwa sana. Namna ya utoaji maamuzi ni tabia
ambayo ukiitumia vizuri inaweza kukusaidia na kukujenga lakini ukiitumia vibaya
inaweza kukuharibia kabisa baadhi ya mambo muhimu.
Jichunguze sasa uone udhaifu
wako kwenye utoaji wa maamuzi uko wapi kisha chukua hatua za namna ya
kujithibiti kulingana na namna unavyohitaji. Ikiwa unatabia ya kutoa maamuzi
haraka haraka na imekuwa ikikugharimu, basi tengeneza utaratibu mzuri wa
kufikiri na kutoa maamuzi.
Afya
Yako Inategemea Tabia Yako
Tabia yako na kanuni zako za maisha zinamchango mkubwa
sana kwenye afya yako. Kama unatabia ya
kula baadhi ya vyakula vinavyoathiri afya yako, kwa asilimia kubwa afya yako
itaathirika. Au kama unatabia mbaya zozote zinazohatarisha afya yako basi kuna
uwezekano kweli afya yako inaweza kuathirika kwa namna moja au myingine.
Siku
moja nilikuwa nazungumza na Mkurugenzi wa kampuni fulani katika mazungumzo yetu ya kawaida akanambia jambo muhimu sana katika
maisha ni afya. Tena akaendelea kusema “Unapokuwa na ndoto za kuanzisha kampuni lako
binafsi, kitu cha kwanza ni kutunza afya yako maana kama afya ilategalega ufanisi
wako katika kampuni utayumba”.
Kuna msemo usemao “afya ni majaliwa ya Mwenyezi Mungu”.
Hilo ni kweli lakini tabia zako zinamchango mkubwa sana kwenye afya yako. Tabia
yako na kanuni zako za kuishi zinaweza kujenga au kubomoa afya yako. Chukua
hatua madhubuti juu ya afya yako mwenyewe.
Fani Yako Na Taaluma Yako Vinaendeshwa Na
Tabia Yako.
Mara nyingi nimeona madaktari bingwa wanavuta sigara.
Lakini akienda mtu mwenye matatizo ya upumuaji utakuta wanamshauri ikiwa ni
mvutaji sigara aache kuvuta sigara! kinachoshanishangaza mbona yeye anayekwambia usivute sigara tena ni
daktari na anajua madhara ya sigara na haachi kuvuta sigara?.
Sio upande wa
madaktari tu bali ni kila fani na taaluma za watu kuna miiko wanaojifunza
inayowakataza kufanya mambo fulani kwa faida yake mwenye fani hiyo mfano
waalimu, wanasheria, wahasibu, nk. lakini tunaona wengi hawatii mafunzo hayo
yenye thamani kwao. Kumbe tatizo ni tabia na kanuni za maisha, mara nyingi
ndizo zinaamua maisha ya mtu huyo yaweje.
Unatakiwa kufanya maamuzi magumu punde unapogundua kuwa tabia
inakupeleka kubaya ni lazima kusema hapana
kwa tabia hiyo. Kutochukua hayo maamuzi magumu kunapelekea kujengeka au
kubomolewa katika misingi sahihi ya mafanikio yako.
Tabia
Yako Hutafuta Watu Wenye Tabia Inayofanana Nayo.
Je, umeshawahi kukaa kwenye kundi la watu wenye tabia
tofauti na wewe? Ulijisikiaje?. Bila shaka ulijisikia mpweke japokuwa umezungukwa
na watu wengi. Sio wewe bali ni tabia yako ilikuwa haifurahii watu wenye tabia
hiyo. Sio kwamba unawachukia bali tabia yako inapiga kelele ndani yako kwa
sauti ile isiyosikika ikisema hapa sio mahala pangu hapa sio mahala pangu. Kwa
kelele hizi za tabia zako utajikuta unakosa amani katikati ya watu hao lakini
utashangaa wenzako wenye tabia zinazoendana wanafurahi na kushangilia.
Jichunguze, huwa unajisikia kuwa na watu wenye tabia
gani? Kama huwa unajisikia vizuri kukaa na watu wanaopenda kuzungumzia
mafanikio basi hilo ni tumaini ipo siku utafanikiwa na kama unapenda kukaa na
watu wasemaji, wenye maneno mengi yasiyofaa ujue kuwa unaharibikiwa maana
mazungumzo mabaya huharibu tabia njema. Chukua hatua mapema juu ya tabia na
mienendo ya maisha yako kwa sababu kuna kujengeka au kubomolewa.
Tabia
Ya Macho na Moyo Ni Mzizi Wa Mambo Mengi.
Macho yanatabia. Yanaweza kufundishwa namna ya
kuangalia na anayeyafundisha macho kuangalia ni moyo. Moyo hufundisha macho na
hudhibiti tabia ya macho. Mfano kipindi mimi nipo mdogo darasa la nne hivi
nilikuwa napenda sana ngoma lakini sikuwa na fursa ya kwenda ngomani maana
nilikuwa bado mdogo hivyo sikuwa naruhusiwa, moyo ulikuwa unaumia sana kwa kukosa
fursa hiyo. Moyo ulikuwa unafurahi sana siku nikipewa nafasi ya kwenda kuona
ngoma hizo, moyo ulikuwa unaridhika ukiona. Kadri nilivyokuwa nakua moyo
uliacha kutamani tena ngoma na kwa sababu hiyo uliyafundisha macho kutopenda
kuangalia ngoma na ndivyo nimekuwa hadi leo.
Bila shaka mpenzi msomaji umeshawahi kukutana na kitu fulani
kikakuvutia sana ukajilazimisha kutokiangalia ila moyo ukaanza kupiga kelele
nataka nikione nataka nikione nataka nikione, usipouzuia moyo utageuka kuangalia
kitu hicho ndivyo tabia ya moyo kuyasakizia macho kuona hata kama jambo
hulipendi kuliona.
Kinachotakiwa ili kuweza kuitawala tabia ya macho na moyo
isiweze kukuvuruga. Unatakiwa kujifunza namna ya kuzishinda tabia za moyo na
macho.
Ziko mbinu nyingi za kushinda tabia hizi mfano kwa kusoma neno la Mungu
na kulitenda katika maisha yako. Chunga moyo wako kuliko mambo yote maana
unaweza kukujenga au kukubomoa.
“Maana
Yale Yanayotoka Nje Ya Mtu Hayawezi Kumfanya Mtu Awe Jinsi Alivyo Bali Maneno
Yale Yanayosema Kwa Sauti Ya Chini Isiyosikika Ndiyo Yanamfanya Mtu Awe Jinsi
Alivyo”.
0 comments:
Chapisha Maoni