Jumatatu, 4 Aprili 2016

Maisha Ni Kama Ujenzi Wa Kiota, Umejenga Chako?

Habari yako ndugu na rafiki;

Leo ni siku nyingine nzuri, yenye kila Neema na Rehema. Najisikia furaha pale ninapokuona tunaendelea pamoja kwenye juhudi zetu za kuboresha maisha yetu. Leo nimekuletea makala hii nzuri ndani yake ikiwa imebeba ujumbe muhimu kwako kwa wakati huu. 

Ndugu, maisha yapo, yataendelea kuwepo hata kama mimi na wewe hatutakuwepo. Mimi na wewe na yule na watu wengine wote unaowaona tumepewa fursa moja kubwa ya kuishi. Wote tumezaliwa na tumekua kila mmoja kwa jinsi yake, wote tunapumua na kutumia hewa hii hii ya aina moja. Wote tunapata mwanga huu huu wa jua. Na mambo mengine mengi tunashirikiana sawa kwa wote.

Pamoja na kwamba tuna shirikiana mambo mengi, kuna tofauti zinajitokeza miongoni mwetu. Moja ya tofauti hizo ni mafanikio. Kuna wengine japo umri na mambo mengi tunafanana lakini wanatuzidi kimafanikio. Kunasababu nyingi ambazo tunaweza kuzitumia kama ndizo zinazosababisha tutofautiane kimafanikio. Hilo lisikutishe, hebu tujifunze kwa viumbe wengine.



Ndege Wajenzi Na Wasio Wajenzi

Kama ilivyo kwa binadamu, ndivyo ilivyo kwa viumbe wengine kama ndege. Wote wanazaliwa, wanakua na hatimaye wanakuwa ndege wakubwa kwa jinsi
yake. 
Bila shaka utakuwa umeshapita hapa na pale ukakuta kiota au viota vya ndege. Kuna baadhi ya ndege wao wamebobea kujenga viota. Hawawezi kuishi bila kuwa na kiota, lakini kuna ndege wengine  hawawezi kujenga kiota wala hawajathubutu kujenga hata kimoja. Unafikiri tofauti ya ndege wanaojenga kiota na wasiojenga kiota ni nini?. 
Usiseme ni mazingira wanayoishi ndiyo yanayowatofautisha hilo sio kweli kwa sababu utawakuta wanaishi eneo moja tena huwa wanawaona wenzao jinsi wanavyojenga lakini bado hawajengi vya kwao. Usiniambie tofauti yao ni umbo kwamba wengine ni wakubwa na wengine ni wadogo kwa umbo, hilo sio kweli mbona tai ni ndege mkubwa lakini anajenga kiota chake na njiwa pori ni wadogo nao wanajenga kiota chao. Kwanini baadhi ya ndege wanamaumbo makubwa kwa madogo lakini hawajengi viota vyao?




Sababu Sita Kwa Nini Baadhi Ya Ndege Hawajengi Kiota Chao.



Sababu ya kwanza: Hawajawahi kuona ndege wa jamii yao wanajenga Kiota. 
Ndege ambao hawajengi kiota sio kwamba hawawezi kujenga ile tu kwamba hata wazazi wao tangu wazaliwe hawajawaona wanajenga kiota, na wakiangalia kwenye ukoo wao hakuna hata mmoja aliyewahi kujenga kiota, basi inawapa imani kwamba hata wao hawawezi kujenga, au wanaamini kwamba kujenga kiota sio utamaduni wao. 
Kwa sababu ya imani hiyo wala hawahangaiki kujifunza jinsi ndege wengine wanavyojenga. Zaidi zaidi wanavizia pale ndege wajenzi wanapohama na wao wanaenda kuingia kwenye viota vya wenzao halafu wanajisikia vizuri tu na wanataga na kutaga mayai humo.



Sababu ya pili: Wanaamini kujenga kiota ni taabu Sana. 
“Kwa nini kuhangaika kutafuta majani ya miti ya kujengea kiota wakati naweza kutembeatembea nikakuta kiota kimejengwa na mwenyenacho hayupo halafu nikaishi humo kiulaini”, hayo ni mawazo ya ndege wasiojenga viota vyao. Kwa sababu ya mawazo hayo na imani hiyo hawahangaiki hata kujifunza namna ya kujenga viota vyao.



Sababu ya tatu: Kwao shida na dhiki watavumilia tu. 
Ndivyo wanavyofanya hata leo. Ikinyesha mvua kubwa wanavumilia kwa kujibanza kwenye matawi ya miti na kwenye mapango. Jua likiwaka sana wanafanya vile vile wanavumilia tu, wakati wa kulala usiku watatafuta tafuta sehemu watajibana usiku utapita. Wao hiyo dhiki ni kawaida wala hawajiulizi njia za kutatua dhiki hizo.



Sababu ya nne: Wanaamini kiota sio muhimu kwao. 
Ingawaje wakitaka kutaga wanavamia viota vya wengine. Kwa lugha nyingine wanajitekenya halafu wanajicheka wao wenyewe. Mimi nawaonea huruma ndege hawa, kwanini wasijenge kiota chao tu halafu wendelee kufurahia maisha?



Sababu ya tano: Mabingwa wa kuongea, kukosoa na kudharau viota vya wengine. 
Ndege hawa ni waajabu sana, saa za kufanya kazi utawakuta wanaimba nyimbo nzuri wakijinadi kwamba wao ndo wababe wa pori.  Wanapowaona wengine wanaojenga viota, wanawakosoa kwa maneno ya dharau na kashifa. Ni mabingwa wa kulinganisha viota vya wenzao huku wao hawajajenga hata kimoja. Ni aibu kuwa na ndege kama hawa.



Sababu ya sita: Mungu amewaruhusu wawe hivyo ili watufundishe. 
Mimi namshukuru Mungu kwa kuwaacha  ndege hao katika hali hiyo japo inauma kuwaona wakiteseka. Alitaka nipate kuona na kuelewa kwamba unaweza kuishi katikati ya fursa zote lakini usijenge kiota chako japo wenzako wanaokuzunguka kila siku wanajenga viota vyao.  Baada ya kuligundua somo hili nimedhamiria kujenga kiota changu. Anza kujenga na wewe cha kwako.



Mfano Huu Wa Ndege Unakuhusu Kwa Namna Hii

Nimesikia mara nyingi watu wakilalamika kuwa mazingira ni magumu ndiyo maana hawajafanikiwa mpaka sasa. Wanatolea mifano ya watu waliofanikiwa wanasema, fulani alifanikiwa kwa sababu baba yake alikuwa tajiri, amempa mtaji mkubwa ndiyo maana sasa hivi amefanikiwa na kutajirika. 
Uwezo wa kufikiri wa watu wanaosema hivyo unaishia hapo. Kinachobaki ni kulalamika na kuilaumu Serikali eti haiwajali, ndivyo wanavyofanya ndege ambao hawajengi viota vyao. 
Kama unajenga kiota chako utaupata wapi muda wa kulalamika?. Mimi sijui kama Serikali haitujali ninachojua, kama Serikali haitujali mbona kunawatu wanatajirika wala hawako kwenye Serikali!, si kwa mali ya wizi bali kwa juhudi zao na maarifa yao?. 
Iache Serikali ifanye ya kwake wewe fanya ya kwako, ukiona Serikali inakubana au haikuungi mkono kwenye njia fulani badilisha njia tafuta njia ambayo utafanikiwa.

Jifunze kujenga kiota chako. Nenda porini au sehemu walipo ndege wanaojenga kiota. Kaa mahali wanapojenga waangalie kwa muda jinsi wanavyojenga kiota chao jifunze kitu harafu rudi kaanze kujenga kiota chako. Ukisahau rudi tena kwenye kiota wanachojenga ndege jifunze kitu halafu rudi ukaendelee kujenga kiota chako. Usiweke visingizio kama wanavyoweka wale ndege wasiojenga viota vyao.



Tumia Udhaifu Ulionao Kufanikiwa

 Tunaweza kujifunza kupitia kwa mwanamama mmoja  mfadhili wa chuo cha SEKOMU kilichopo mkoani Tanga. 

Mama huyu Lena Maria hana mikono tangu kuzaliwa kwake, pia mguu mmoja hauko vizuri, pamoja na ulemavu huo amesafiri dunia nzima akitoa matumaini kwa watu waliokata tamaa, kwa sababu pamoja na ulemavu huo ameweza kushinda medali ya dhahabu mwaka 1989 kwenye mashindano ya kuogelea ya Olympic. Sio hilo tu anaweza kuendesha gari kwenye majiji makubwa kama vile Tokyo kwa kutumia miguu yake. 
Kwa sasa ni tajiri mkubwa ndiye miongioni wa watu waliokifadhili chuo kikuu cha SEKOMU.  
Je, ningekuwa mimi au ungekuwa wewe ungeweza kufanya nini ukiwa katika hali hiyo? Acha kuwa ndege asiyejenga kiota anza kujenga kiota chako, nakushauri anza leo kwa kuchukua maamuzi sahihi. Udhaifu ulionao ubadilishe ukutie nguvu ya kufanikiwa zaidi.



Unaanzi Wapi Sasa.

Kwanza jifunze kutengeneza pesa, ongeza ufahamu na maarifa akilini, usianze kwa kutumia nguvu anza kwa kuongeza ufahamu.Ufahamu utaupata kwa kusoma vitabu na kuongea na watu walioanza kujenga viota vyao.


Unaweza kuishi katikati ya fursa zote lakini usijenge kiota chako japo wenzako wanaokuzunguka kila siku wanajenga viota vyao.  Baada ya kuligundua somo hili nimedhamiria kujenga kiota changu. Anza kujenga na wewe cha kwako”

0 comments: