Jumatatu, 1 Februari 2016

UKATILI WA KIJINSIA

AINA ZA UKATILI WA KIJINSIA
UKATILI wa kijinsia ni jambo kubwa kwenye ajenda za haki za binadamu kimataifa, na unaweza kuwapata wanaume, wanawake na watoto ambao ndio waathirika wakubwa.
Hali hii inatokana na mifumo mbalimbali iliyopo na uhusiano wa kijinsia ulivyo katika jamii zetu hapa nchini ambapo jinsi moja hujiona ni bora kuliko
nyingine.
Kwa miaka mingi mwanaume amechukuliwa kuwa daraja la juu kuliko mwanamke katika nyanja zote za kijamii, kiutamaduni, kisiasa na kiuchumi.
Utaratibu huu umejengwa tangu enzi na enzi katika ngazi ya familia hadi taifa.
Kuna aina tofauti za ukatili wa kijinsia na hii inategemeana na utamaduni na historia ya jamii husika.
Mara nyingi ukatili huu hufanyika kati ya wanandoa au wapenzi. Hata hivyo wanawake wamekuwa wakisumbuliwa zaidi na ukatili wa kijinsia katika uhusiano huo.
* Ukatili wa kimwili.
Ukatili wa kimwili ni kitendo anachofanyiwa mtu kinachohusisha kuumizwa mwili na huweza kuonekana moja kwa moja.
Wakati mwingine mtendewa ukatili anaweza kuyahisi maumivu bila mtu mwingine kutambua kuwa amefanyiwa ukatili wa kimwili.
Baadhi ya mifano ya ukatili kimwili ni pamoja na vipigo, shambulio la mwili, kuchomwa mwili moto, matumizi ya silaha, kuvuta nywele, kusukuma, kumpiga kichwa ukutani na kuchomwa na kitu chenye ncha kali sehemu yoyote mwilini.

* Ukatili wa kisaikolojia.
Ni ukatili ambao mtu anatendewa na unamsababishia maumivu kihisia, ambapo mtu mwingine hawezi kutambua kuwa mwenzake ametendewa ukatili hadi mazingira yatakapojitokeza na mtendewa akajieleza.
Mifano ya ukatili wa aina hii ni pamoja na matusi kwa njia ya maneno au ishara yenye lengo la kudhalilisha, vitisho na kutishia kufanya fujo, maneno ya kufedhehesha, kudharauliwa hadharani, kutishia kutoa siri, kuingiliwa faragha, kutishiwa kuuawa, wivu wa kupindukia ama kunyang’anywa watoto kwa makusudi.

* Ukatili wa uhusiano wa kingono.
Ukatili huu huambatana na vitendo vinavyohusiana na masuala ya ngono.
Kwa mfano bughudha za kijinsia, kujamiiana kwa maharimu, ubakaji ndani ya ndoa, ulawiti, utekaji na usafirishaji wa wanawake au wanaume na watoto kwa ajili ya ngono, utumwa wa kingono, mashambulio na kuingiza vitu vigumu kwenye sehemu za siri.
Vitendo vingine ni kujaribu kulazimisha ngono, kuweka mazingira ya ngono isiyo ya ridhaa au ubakaji, kupima ubikira, kulazimisha kutoa mimba, kukataza matumizi ya utaratibu wa kuzuia mimba, kulazimisha mimba, kulazimisha ngono bila kujali kuambukiza magonjwa na kulazimishwa kufanya biashara ya ukahaba.

* Ukatili wa kiuchumi.
Ukatili wa kiuchumi ni aina ya ukatili ambayo inamnyima fursa za kiuchumi mwanamke au mwanaume katika kujiongezea kipato na kuchangia katika maendeleo.
Aina hii ya ukatili huwapata wanawake kutokana na hali yao ya kuwa tegemezi kwa wenzi wao.
Kitendo cha wanawake kuwa tegemezi kwa wanaume kinawaathiri sana kwani wanakosa kauli katika mali za familia na hawashirikishwi katika uamuzi wa maendeleo.
Waaathirika wakubwa wa aina hii ya ukatili ni wanawake na wasichana.
Mifano ya ukatili wa kiuchumi ni kama vile kunyang’anywa mali, ubaguzi katika fursa za kujipatia mahitaji muhimu kama chakula, malazi na mavazi, kunyimwa haki za kurithi, elimu duni na mianya finyu ya fursa za kujielimisha, kunyimwa sehemu ya mapato ambayo ni jasho lako na kukatazwa kufanya kazi.

* Ukatili wa mila potofu. Ukatili huu unatokana na mila na desturi za jamii zetu ambazo zinakinzana na haki za binadamu, hivyo kuchangia kuwepo kwa vitendo vya ukatili wa kijinsia.
Baadhi ya mifano ya ukatili wa kijinsia unaotokana na tamaduni au mila potofu ni kama vile ndoa za kushurutisha, ndoa za utotoni, kutakasa wajane, kurithi wajane, ukeketaji, matambiko ya kingono kwa watoto, ndoa za maharimu, kufungiwa au kuwekwa ndani kwa shuruti, ndoa za ushirika, miiko ya chakula na ukatili utokanao na mahari.

* Mahali pa kupata msaada.
Mwathirika hana budi kutafuta msaada kwa mtu anayemwamini au kuripoti polisi. au wasiliana na
TABORA NEW HOPE AGENY (TANEHA) +255 753 062 458 AU +255 762 336 533

5 comments:

Husnat Mourick alisema ...

Kwani mashirika na taasisi za kiserikali na zisizo za kiserikali wana deal na wanawake pekee kama ndio kundi pekee linalonyanyasika?
mimi nina uhakika kuwa hata wanawake pia wanawanyanyasa sana wanaume lakini wanaume wachache sana wenye ujasiri wa kujitokeza na kutoa malalamiko.
Hivyo maoni yangu ni kuwa muwajengee uwezo na wanaume ili kuwapa ujasiri wa kujitokeza kutoa malalamiko yao.

Paul D. Kisyala alisema ...

ni kweli wanawake wanaonekana kunyanyasika zaid kwa kuwa wao wanaujasiri mkubwa sana wa kulalamika tofauti na sisi wanaume ambao wengi wanaona ni aibu kubwa kulalamika kuwa wananyanyaswa na wake zao.
TANEHA fanyeni mkakati wa kuwajengea uwezo na wanaume!!

Bila jina alisema ...

Kuna rafiki yangu mmoja anatumikia kifungo gerezani kwa sababu ya kumfanyia ukatili mkewe kwa kumjeruhi vibaya, lakini nilipomtembelea gerezani alinisimulia jinsi ambavyo mkewe alikuwa akimnyanyasa kisaikolojia kwa muda mrefu na alishindwa kuvumilia zaidi pale alipogundua kuwa mkewe anamnyanyasa kwakuwa ana bwana mwingine mwenye uwezo mkubwa ambaye mkewe alimtamkia wazi kuwa hata mtoto wao mdogo alikuwa ni wa yule jamaa wa nje.
sasa kama rafiki yangu angekuwa na ujasiri wa kujitokeza na kupata ushauri pengine asingejikuta yuko gerezani.

TANEHA Toeni elimu

Mwalimu Mgunda alisema ...

ukatili ni janga kubwa sana haswa kwa huku vijijini ni balaa sana.
Tutembeleeni huku wilaya ya Uyui,Tabora mtusaidie

Unknown alisema ...

Ahsanteni sana wadau kwa maoni yenu. Tunaahidi kuyafanyia kazi kwa uzito wa kipekee.
endeleeni kutupa maoni yenu kila mpatapo nafasi.

With thanks
Dennis John Kumwenda - Executive Secretary