SERIKALI imesema asilimia 15 ya wanawake nchini wamekeketwa, huku mikoa mitano ikiwa imekithiri kwa vitendo hivyo.
Mikoa hiyo na asilimia ya ukeketaji kwenye mabano ni pamoja na
Manyara (71), Dodoma (64), Arusha (59), Singida (51), na Mara (40).
Akizungumzia maadhimisho ya siku ya ukeketaji leo kwa niaba ya waziri
wa Afya, maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto, Katibu Mkuu wa
wizara hiyo, Sihaba Nkinga alisema vitendo vya ukeketaji bado
vimeshamiri nchini.
“Ukatili huu wa ukeketaji umekuwa ukijidhihirisha katika sura
mbalimbali zikiwemo za baadhi ya makabila kuhalalisha vitendo hivyo kwa
kisingizio cha mila na desturi za kabila husika,” alisema Nkinga.
Alisema ukeketaji ni udhalilishaji wa wanawake na watoto wa kike na
huhatarisha maisha yao, lakini vitendo hivyo vinaendelea kufanyika kwa
siri katika jamii huku madhara yake yakiwa ni vifo, vilema na maradhi
kama fistula.
Nkinga alisema mbali na kuwepo kwa mwamko kutoka kwa jamii wa
kuripoti matukio ya vitendo hivyo bado ipo kazi kubwa ya kufanya kwa
kuwa suala la kubadili fikra na mitizamo ya jamii haiwezi kuisha kwa
siku moja kwa kuwa vitendo hivyo bado vinaendele kutokea.
Kuhusu maadhimisho, alisema kitaifa yatafanyika mkoani Singida huku
mikoa mingine ikiadhimisha kwa matukio kadha wa kadha lengo likiwa ni
kuongeza uelewa kwa jamii ili kutokomezwa kwa ukeketaji nchini.
Jumamosi, 6 Februari 2016
ASILIMIA 15 YA WANAWAKE NCHINI WAMEKEKETWA - SERIKALI
2:24:00 PM
No comments
0 comments:
Chapisha Maoni